Je Mwivi Katika Yohana 10:10 Ni Nani?

JE MWIVI KATIKA YOHANA 10:10 NI NANI?

Biblia inatakiwa kusomwa kwa kufuata MUKTADHA, yaani mfululizo au mtiririko wa mawazo/habari. Mstari wa Biblia ukitolewa kwenye muktadha unaweza kuwa na maana yoyote anayotaka msomaji, kitu ambacho si sawa. Kusoma kwa muktadha si rahisi kama ambavyo tunaweza kusema. Kwa nini ni ngumu? Mara nyingi tunapoiendea Biblia huwa tunakuwa na majibu tayari tunayoyajua kwa kuyasikia kwa watu, hivyo ni rahisi kujisoma mwenyewe kuliko kusoma Biblia.

Biblia katika Yohana 10:10 inasema “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.”

Bila shaka, Biblia imeeleza kile ambacho mwivi anafanya, lakini haijamtaja mwivi ni nani katika mstari huo. Mstari wa kwanza wa Yohana 10 pia unaeleza kuhusu mwizi. Mstari wa Kwanza unasema, “Yesu aliwaambia, Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi.” (Yohana 10:1)

Mstari wa nane wa sura hii hii pia Yesu anaelezea kuhusu mwivi, lakini sasa kwa wingi:
“Wote walionitangulia ni wevi na wanyang’anyi; lakini kondoo hawakuwasikia.” (Yohana 10:8)
Yesu hapa anajiweka upande wa Mchungaji wa kondoo, na kundi la pili ni la mwivi au wevi. Zaidi ya hilo, kundi hili la pili linatajwa kwa kutumia maneno mengine zaidi ya “mwivi” tu; anasema pia “mnyang’anyi” au “wanyang’anyi.”

Katika mstari wa kumi na mbili wa sura hii hii, Yesu anaongeza kueleza sifa za hawa wevi au huyu mwivi. Anasema:
“Mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia; na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya.” (Yohana 10:12)

Ukisoma vizuri, utagundua Yesu anajielezea Yeye kama mchungaji mwema kwa kuwa atautoa uhai wake kwa ajili ya kondoo. Lakini upande wa pili, anasema hawa wevi au huyu mwivi hawajali kondoo kwa kuwa si mali zao/yake, na zaidi, wakiona mbwa-mwitu wanakimbia. Hii yote ni lugha ya picha Yesu anayotumia, akijiita mchungaji mwema, na kundi ambalo liko kinyume naye ni wevi, wanyang’anyi, na ni watu wa mshahara.

Kwa nini Yesu anatumia lugha hii ya picha?

Yesu amejifunza Maandiko tangu akiwa mtoto, hivyo hata mifano yake au lugha yake ya picha haiendi mbali na Maandiko. Yesu anatumia lugha ya picha iliyotumika katika Ezekieli 34. Katika Ezekieli 34, Mungu anamwambia Ezekieli atoe onyo kwa wachungaji wa Israeli, yaani viongozi wa dini ya Kiyahudi, kwa kuwa hawafanyi kama Mungu anavyowataka wafanye (soma Ezekieli 34 kuelewa vizuri). Lakini Mungu haiishii kutoa onyo tu, bali anatoa ahadi kwamba iko siku Yeye mwenyewe atakuja kwa ajili ya kuwalisha kondoo wake. Maandiko haya yanasema;

Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu ya wachungaji; nami nitawataka kondoo zangu mikononi mwao, nami nitawaachisha hiyo kazi ya kuwalisha kondoo; nao wachungaji hawatajilisha wenyewe tena; nami nitawaokoa kondoo zangu vinywani mwao, wasiwe tena chakula chao.  Maana, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi, nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia. Kama vile mchungaji atafutavyo kondoo zake, siku ile anapokuwa kati ya kondoo zake waliotawanyika; ndivyo nitakavyowatafuta kondoo zangu; nami nitawaokoa katika mahali pote walipotawanyika, katika siku ya mawingu na giza.  Nami nitawatoa katika watu wa mataifa, na kuwakusanya katika nchi zote, nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe; nami nitawalisha juu ya milima ya Israeli, kando ya mifereji ya maji; na katika mahali pote pa nchi panapokaliwa na watu. Nami nitawalisha malisho mema, pa juu ya milima ya mahali palipoinuka pa Israeli litakuwa zizi lao; huko watalala katika zizi jema; nao watakula malisho mema, juu ya milima ya Israeli. Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana MUNGU.Nami nitawatafuta waliopotea, nitawarudisha waliofukuzwa, nitawafunga waliovunjika, nitawatia nguvu wagonjwa; nao wanono na wenye nguvu nitawaharibu; nitawalisha hukumu.” (Ezekieli 34:10-16)

Mungu anaahidi kwamba iko siku atakuja Yeye Mwenyewe kuwalisha kondoo wake wa Israeli. (Hii ndiyo maana Yesu anasema anao kondoo ambao si wa zizi hili—zizi likiwa ni Israeli—akiashiria kwamba kuna kundi lingine mbali na Waisraeli ambalo lipo katika zizi lake la sasa, yaani mataifa).

Mungu atawachunga Kondoo wake yeye mwenyewe kwa namna gani?

Katika sura hii hii, Mungu anaeleza kwa namna gani atakuja kuwachunga kondoo wake Israeli, yeye mwenyewe. Mungu anasema;

Nami nitaweka mchungaji mmoja juu yao, naye atawalisha, naam, mtumishi wangu, Daudi; yeye atawalisha, naye atakuwa mchungaji wao. Na mimi, Bwana, nitakuwa Mungu wao, na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mkuu kati yao; mimi, Bwana, nimesema haya. Nami nitafanya agano la amani nao, nami nitawakomesha wanyama wakali kati yao; nao watakaa salama jangwani, na kulala misituni.” (Ezekieli 10:23-25)

Kwa kusoma maandiko hayo unaweza kujiuliza, Atamuweka Mchungaji mmoja, Mtumishi wake Daudi? Daudi mbona alikuwa ameshakufa zamani wakati wa Ezekieli?

Kuna mengi ya kujifunza hapo, lakini Mungu alikuwa anamaanisha Masihi (ambaye atatoka katika uzao wa Daudi) ndiye atakayekuwa mchungaji juu ya kondoo wa Israeli. Na wale wote wachungaji wasiofanya kama alivyowapa kufanya, hawatakuwa na nafasi ya kuwasumbua kondoo. Kwa Ezekieli, wachungaji sio shetani, bali ni viongozi wa dini ya Kiyahudi ambao walikuwa wanafanya tofauti na Mungu alivyotaka wafanye.

TURUDI YOHANA 10

Habari ya Yohana 10 inaanzia Yohana 9. Katika Yohana 9, habari inaanza Yesu anamponya kipofu tangu kuzaliwa, lakini mafarisayo (viongozi wa dini ya Kiyahudi) wakamsumbua kipofu na wazazi wake kwa kuwa walikuwa hawamwamini Yesu kama ndiye Masihi.

Usumbufu huu sio wa kumwita tu mara nyingi kumuuliza kuhusu Yesu, bali nyuma yake usumbufu huu ulikuwa na agenda ya kutaka kujua kama kipofu anamwamini Yesu kuwa ndiye Masihi, na wao walikuwa wamekubaliana kuwa atakaye mkubali Yesu kuwa ndiye Masihi atatengwa na sinagogi (kipofu alimwamini na mpaka kumwabudu).

Hivi ndivyo Yohana anavyoripoti:
“Wazazi wake waliyasema hayo kwa sababu waliwaogopa Wayahudi; kwa maana Wayahudi walikuwa wamekwisha kuafikiana kwamba mtu akimkiri kuwa ni Kristo, atatengwa na sinagogi.” (Yohana 9:22)

Hivyo, mzozo ulikuwa kati ya Yesu na mafarisayo (viongozi wa dini waliokuwa wanafanya tofauti na Mungu anavyotaka).

Kwa kuwa Yohana 10 ina muktadha huu wa kutoka sura ya 9, Yesu anapoanza kuzungumza katika sura ya 10, anazungumza kutokana na tukio la sura ya 9. Anawasema mafarisayo (viongozi wa dini wa Kiyahudi) kuwa ni wanyang’anyi na wevi kwa sababu ya mambo wanayoyafanya. Lakini hawasemi kwa wazi bali anawasema kwa kutumia lugha ya picha kama ambavyo Mungu alizungumza na viongozi wa dini wa Kiyahudi kwa kutumia kinywa cha mtumishi wake Ezekieli. Hivyo, Yesu katika Yohana 10:10 anajitofautisha na mafarisayo kwa kutumia tukio la kondoo (Kipofu na wale wanao mwamini). Kwa muktadha huu Yesu ahajitofautishi yeye na shetani bali anajitofautisha yeye na mafarisayo.

Je, ni mafarisayo tuu ndio Yesu alimaanisha kuwa wevi na wanyang’anyi? Jibu si wao tu, bali viongozi wote wa kidini waliokuwa wanafanya kinyume na Mungu alivyowaaagiza. Tangu awali, walikuwepo viongozi wa dini wa Kiyahudi ambao walifanya tofauti na Mungu alivyotaka, na Mungu alishawaonya.

Hivyo, katika Yohana 10:10 (pamoja na Yohana 10:1 na 10:8), mwivi/wevi ni viongozi wa dini ya Kiyahudi wanaofanya mambo tofauti na maagizo ya Mungu, na sio shetani kama wengi wanavyodhani.

SISI LEO TUNAJIFUNZA NINI?

Kwa kuwa hili ni Neno la Mungu kwa ajili yetu, ni vizuri kujua kwamba linasema na sisi leo kama lilivyosema na watu wa karne ya kwanza. Andiko hili lina uzito wa milele, na kwetu leo linatufundisha umuhimu wa kutambua wevi na wanyang’anyi—yaani, viongozi wa dini ambao wanafanya mambo tofauti na maagizo ya Mungu.

Tutawatambuaje? Kwa kuangalia sifa zao ambazo Yesu alizitaja mwenyewe.

Yesu anasema kuwa hawa ni watu wa mshahara—watu wanaojihusisha na uongozi sio kwa upendo kwa kondoo, bali kwa ajili ya faida binafsi.

Ni watu ambao, wakiona mbwa mwitu anakuja, hukimbia na kuwaacha kondoo bila ulinzi, wakionyesha kuwa hawaoni kwamba usalama na afya ya kondoo kuwa ni jukumu lao la kweli. Pia ni watu ambao malengo yao katika kazi ya uongozi ni kuiba, kuchinja na kuharibu—yaani, hawajengi, bali wanavuruga, wanapotosha na kuangamiza ili mradi tu wao wafaidike.

Hili andiko linatufundisha kuwa makini, kutotazama tu sura ya nje au umaarufu wa viongozi wa kidini, bali kuchunguza matendo na tabia zao kulingana na vigezo ambavyo Yesu mwenyewe ametupatia. Katika kufanya hivyo, tutakuwa wakweli kwa sauti ya Mchungaji Mwema na tutaepuka uharibifu wa wale wanaokuja kwa sura ya huduma lakini mioyo yao imejaa tamaa na ubinafsi.